Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi Bw. Gabriel Migire amesema Kwa sasa Biashara ya Usafirishaji ka njia ya maji katika Bara la Afrika imekuwa ikikuwa kutokana na mizigo mingi inayosafirishwa duniani inatoka na kuja Afrika.
Bw. Migire ameyasema hayo leo Februari 27, 2023 wakati wa Mkutano wa Taasisi inayojihusisha na masuala ya usafirishaji wa majini (ISCOS), uliofanyika katika hoteli ya Four Points jijini Dar es salaam.
“Sisi kama Waafrika tuna kila sababu ya kuhakikisha tunakuwa na watu wanamiliki vyombo vya usafiri majini”.
Aidha amesema kuna changamoto ya ukosefu wa vyombo vya kujifunzia kwa upande wa wanafunzi wanaosoma Chuo cha Bahari (DMI) pindi wanapomaliza mafunzo hayo ya ubaharia.
“Tunahitaji kuwa na vyombo vyetu lakini pia tunahitaji vyombo hivi kwa ajili ya kufanya biashara kwa sababu Afrika sasa hivi inafunguliwa kibiashara” Amesema Bw. Migire.
” Sisi kwenye eneo hili la Afrika Mashariki na ISCOS member state tunakila sababu ya kuhakikisha kwamba tunatumia hiyo fursa ya kushiriki kwenye hiyo biashara ya Afrika, Tunavyofunguliana nchi za Afrika haina maana kwamba turuhusu mabara mengine yaje tafanye biashara Afrika ,ni sisi nchi za Afrika tunatakiwa kuhakikisha tunatumia hiyo fursa” Ameongeza Bw. Migire.
Kwa upande wake Katibu mkuu wa ISCOS, Daniel Kiange amesema kwa sasa Wakati umefika wa Afrika kuweza kuwa na vyombo vya usafirishaji ili kurahisisha usafirishaji wa bidhaa kwenda ughaibuni.
“Tuweze kuwa na meli zetu ambazo zinaweza kubeba mizigo kwenda China,South Africa na kule kwingine ili hiyo pesa iweze kubaki katika Kanda yetu, na pia tuweze kutengeneza nafasi za kazi kwa ajili ya vijana wetu” Amesema Kiange.
Naye Katibu Mtendaji wa chama cha wamiliki wa meli barani Afrika (African Shipowners Association), Bi.Funmi Folorunso amesema kufuatia mkutano huo wanatarajia Nchi Wananchama wa ISCOS watakuja na sera ya umiliki wa meli katika kusaidia sekta ya usafirishaji.
Godwin Isdore kutoka Songoro Marine ni mmoja wa wadau walioshiriki mkutano huo amesema ni kushiriki katika mkutano huo ni ya kuongeza maarifa pamoja na kujenga uhusiano na wadau kutoka nchi wanachama wa Iscos wakiwemo kutoka Kenya na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
“Tukiangalia katika Afrika , moja kati ya biashara kubwa inayofanyika ni Shipping na kama unavyoona wadau wameamka na wanasema ni muda sasa wa kumiliki meli” Amesema Godwin.
Intergovernmental Standing Committee on Shipping (ISCOS) ni taasisi inayojihusisha na masuala ya usafirishaji wa majini ambayo kwa sasa inazijumuisha nchi za TANZANIA, KENYA, UGANDA ZAMBIA na DRC.